Kikosi cha FFU uwanjani. Jeshi la polisi mkoani Morogoro limekanusha madai ya kuhusika na kumpiga risasi begani, katibu wa jumuiya na taasisi ya kiislamu nchini, sheikh Ponda Issa Ponda, na kwamba iwapo sheikh huyo anaamini kufanyiwa hivyo, ajitokeze na kuthibitisha kauli hizo ambazo zimeendelea kutolewa na wafuasi wake.
Akizungumzia tukio la vurugu zilizojitokeza baada ya kufanyika kwa 
mhadhara wa baraza la Iddi, lililoandaliwa na wahadhiri wa kiislamu wa 
mkoa wa Morogoro eneo la Kiwanja cha ndege,na baadaye kuzagaa kwa 
taarifa kuwa sheikh Ponda amepigwa risasi na kujeruhiwa, kamanda wa 
polisi mkoa wa Morogoro Faustine Shilogile, amesema saa chache kabla ya 
mhadhara kumalizika, sheikh Ponda  alijitokeza na kuzungumza na 
wananchi, na baadaye kuondoka na gari, akisindikizwa na kundi la wafuasi
 wake waliokuwa kwa miguu, lakini polisi walimzuia kwa mbele katika 
barabara ya Tumbaku, kwa nia ya kutaka kumkamata kutokana na tuhuma za 
uchochezi katika mikoa ya Dar es Salaam na Zanzibar, jambo 
lililosababisha wafuasi hao kuwazuia polisi kwa mawe na kusababisha 
watumie risasi baridi kupiga hewani kuwatawanya.
Kuhusu kushindwa kumkamata sheikh Ponda wakati akiwa jukwaani, 
Shilogile amesema ilikuwa ni kuepusha vurugu ambazo zingeweza 
kujitokeza,ambapo mkutano huo ulihudhuriwa na watu zaidi ya 3,000 .
Wakizungumza katika hospitali ya rufaa ya mkoa wa morogoro,baadhi 
ya wazazi waliolazwa na watoto katika wadi namba 06, wamesema Jumamosi 
jioni vurugu kadhaa zilijitokeza baada ya kuwasili kwa majeruhi sheikh 
Ponda hospitalini hapo,ambapo kabla ya kupata huduma, aliondolewa na 
watu waliokuwa na pikipiki.
Habari kutoka vyanzo mbalimbali ikiwemo kwa wafuasi wake na 
waandaaji wa mhadhara huo, zimebainisha kuwa sheikh Ponda anaendelea 
vyema jijini Dar es Salaam alikopelekwa,baada ya zahanati mbili tofauti 
alizopelekwa awali kuonekana kukosa huduma zilizomstahili,na alipewa 
 huduma ya kwanza ya kuongezewa maji na damu akiwa kwenye gari, na 
baadae kuondolewa risasi mbili anazodaiwa kupigwa kwenye bega.
 

 
No comments:
Post a Comment